Kitabu hiki cha Sheria

July 19, 2022 in Mwongozo wa Ibada by TGVS

 

Mwongozo wa Ibada/ 6-BSG-1A, (Yoshua 1:7-8)/ Dhamira: Kitabu hiki cha Sheria/ Wimbo: Nipe Biblia (SDAH 272).


Uchunguzi: Kitabu cha Sheria – (Kumb 31:24-26; Kumb 28:58-61; 29:18-21; 30:10; 2 Flm. 14:6; 2 Nya. 17:9; 25:4).

Tafakari: Katika sura hii, tuna mambo yafuatayo: Utangulizi: Uchunguzi wa historia ya Israeli kutoka Misri hadi Kanaani (1-2); Amri ya Mungu kwa Yoshua (3–9); Maagizo ya Yoshua ya kuvunja kambi (10–11); Agizo la Yoshua kwa makabila ya Ng’ambo ya Yordani (12–15); na jibu la Israeli wote (16–18). Kwa utangulizi wa kina wa Yoshua na maelezo ya msingi wake, angalia kipengele cha ‘6-BSG-1J’ kwenye mwongozo huu. Hapa, tutashughulika na aya ya 8 pekee. Musa aliandika Kitabu cha Sheria. Kitabu hiki kilipitishwa kutoka kwa Musa hadi kwa Yoshua (Yos. 1:7-8; 8:30-31,34-35; 23:6; 24:26). Kiligunduliwa tena na kutumika katika utawala wa Yosia (2 Flm. 22:8-16; 2 Nya. 34:15-24). Kilisomwa hadharani na Ezra (Neh. 8:1-18; 9:3). Mtume Paulo pia alirejelea Kitabu cha Sheria, kwa mfano, alipofundisha kwamba kuhesabiwa haki hufanyika kwa imani! (Gal 3:10, cf. Kumb 27:26).

Kitabu cha Sheria ni nini? Pentatuki. “Wakati wa miaka ya uongozi wake, Musa aliweka kumbukumbu iliyoandikwa ya maneno na matendo ya Mungu na kisha kumbukumbu hii akawakabidhi makuhani watunze (Kumb. 31:9). Aliandika ndani yake ukumbusho kwa Yoshua kuwafutilia mbali Waamaleki (Kut. 17:14). Mbali na mambo mengine, “Kitabu cha Sheria” kilijumuisha “Kitabu cha Agano” (24:4, 7), kumbukumbu ya safari za watu hao kutoka Misri hadi Kanaani (Hes. 33:2), maagizo maalum yanayohusu urithi (36:13), na wimbo ambao Musa aliwafundisha watu (Kumb. 31:19). Musa aliendelea kuongeza taarifa kwenye rekodi hii hadi ikajumuisha kila kitu ambacho Mungu alitaka ndani yake (v. 24). Tuna sababu ya kuamini kwamba Vitabu vyote vitano vya Musa (Mwanzo hadi Kumbukumbu la Torati) viliunda “Kitabu cha Sheria,” hiba kuu zaidi ambayo Musa angeweza kumwachia mrithi wake.

Lakini haikutosha makuhani kubeba na kulinda kitabu hiki cha thamani; Yoshua alipaswa kutumia muda kukisoma kila siku na kukifanya kuwa sehemu ya utu wake wa ndani kwa kukitafakari (Zab. 1:2; 119:97; angalia Kumb. 17:18–20). Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “tafakari” linamaanisha “kunong’ona.” Ilikuwa desturi ya Wayahudi kusoma Maandiko kwa sauti (Matendo 8:26–40) na kujinenea binafsi mambo yao na kuyazungumza wao kwa wao (Kumb. 6:6–9). Hii inaeleza kwa nini Mungu alimwonya Yoshua kwamba Kitabu cha Sheria kisiondoke kinywani mwake (Yos. 1:8).” – [Warren W. Wiersbe, Be Strong, “Be” Commentary Series, (Wheaton, IL: Victor Books, 1996), 27–28].

Maana ya Kiibada: Kuna kanuni tatu kuhusu kutafakari neno la Mungu kulingana na Yoshua 1:8. Kwanza, sehemu ya udaima: “Mchana na Usiku” (1:8a). Tafakari hii lazima ifanyike kimwendelezo, na si kwa vipindi kadha wa kadha. Pili, sehemu ya kujisalimisha: “hakikisha unatii kila kitu kilichoandikwa humo” (1:8b, NLT). Kutafakari kunakuza utii na kujiweka wakfu. Tatu, sehemu ya mafanikio: “Ndipo tu utakapostawi na kufanikiwa katika yote uyafanyayo” (1:8c, NLT). Mafanikio haya yanapaswa kueleweka kama mafanikio ya kiroho, si ya mali au ya kifedha.

Sheria (Maandiko) ndiyo chanzo cha ustawi wa kiroho wa mtu husika. Mtu anayetafakari Sheria ya Mungu anafananishwa na “miti iliyopandwa kando ya mto, inayozaa matunda kila msimu. Majani yao hayanyauki kamwe, na hufanikiwa katika yote wafanyayo.” (Zaburi 1:2–3, NLT). Wapendwa, ikiwa tungechukua sura moja baada ya nyingine (au kifungu cha Kimaandiko) na kutumia wakati wetu kujifunza, kutafakari, “tukiufunga ulimwengu na kumruhusu Mungu aseme nasi na kuelekeza akili zetu, tungegundua kweli za ajabu ambazo hatujawahi kuziota humo.” – (SDA BC 2:178). Wapendwa, Neno la Mungu ni jema (Rum. 7:12; 1 Tim 1:8); kamilifu (Zab. 19:7; 119:142; Yak. 1:25) na lidumulo milele (Zab. 119:89).

Mtunzi wa Zaburi anasema, “Neno Lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.” (Zaburi 119:105, cf. Zab. 119:130; 2 Pet 1:19). Neno la Mungu limekusudiwa kutuongoza kwenye wokovu (2 Tim 3:14-15; Zab. 19:7-11; Yn. 20:30-31; Rum. 10:8). Neno la Mungu lina uwezo wa kubadilisha maisha yetu (Ebr. 4:12-13), na kutusafisha (Yn. 17:17). Neno la Mungu hufundisha, hukemea, husahihisha (Zab. 19:11-13; 1 Kor. 10:11-12), na kutupatia mafunzo yahusuyo haki (2 Tim 3:16). Wapendwa, ni lazima, basi, kuingiza nafsini mwetu “Kitabu hiki cha Sheria” kwa kukisoma na kukitafakari (cf. Yos 1:8; Zab. 1:2; 119:97). Kama Mtunzi wa Zaburi, hebu tuseme, “Moyoni mwangu nimeliweka neno Lako, nisije nikakutenda dhambi” (Zab. 119:11). Amina?

Sauti ya Injili: Sehemu hiyo imeandikwa kana kwamba Mungu anazungumza nawe moja kwa moja — kwa sababu Yeye anafanya hivyo. Bwana ananiambia nini asubuhi ya leo? Mwanangu, nilimpa Yoshua amri ileile niliyowapatia wafalme wa baadaye wa Israeli (katika Kumb. 17:19)— kila siku, alipaswa kutafakari kila neno katika “Kitabu cha Sheria” (Yos 1:8). Unapofanya mapenzi Yangu (kwa namna Yangu, kwa msaada Wangu), hakuna chochote na hakuna yeyote anayeweza kukuzuia katika njia ya mafanikio yako. Bado, ufunguo ni utii kwa Neno Langu (Yos 1:5). Je, unataka kujua mapenzi Yangu kwako? Je, unataka kuwa mshindi juu ya dhambi, dhiki, na majaribu ya maisha haya? Je, unataka kuishi kwa haki katika “kizazi chenye ukaidi na kilichopotoka” (Filp. 2:15)? Basi ingia katika Neno: lisome, litii, na ufungue moyo wako Roho auongoze. Nitakubariki na kukupeleka maeneo ambayo kamwe usingeweza kufikiria! Je, utafanya hivyo?

Shauku Yangu: Kwa neema ya Mungu, nataka kufurahia Sheria ya Bwana na kuitafakari mchana na usiku!

Uwe na Siku Yenye Baraka: “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.” (Yoshua 1:8)


 

Ibada Kupitia Uimbaji: Nipe Biblia (SDAH 272).

 

Comments